TAARIFA KAMILI MAJAMBAZI KUVAMIA KITUO CHA POLISI WAKIWA NA SILAHA ZA KIVITA,KUUA ASKARI 2,KUIBA SILAHA


 Majambazi wameingia na kuvamia kituo cha polisi Wilaya ya Bukombe Mkoani Geita kisha kuua askari wawili, kujeruhi wengine wawili  kisha kupora bunduki kumi risasi na mabomu ya mkono kisha kutokomea pasipo kukamatwa.
Tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia leo ambapo majambazi hao walivamia katika kituo kikuu cha polisi Wilaya ya Bukombe Mkoani saa 9 alfajiri wakiwa na silaha za kivita na mabomu ya kurusha kwa mkono.


Mwandishi wa Malunde1 blog Victor Bariety anasema kwa mujibu wa taarifa alizozipata ni kwamba majambazi hao walizingira kituo hicho hadi eneo la mapokezi(CRO)na kuanza kuwamiminia risasi za moto askari waliokuwa zamu.

Kufuatia hali hiyo askari wawili kati ya wanne waliokuwa kituoni hapo walipoteza maisha huku wengine wakijeruhiwa vibaya sehemu mbalimbali za miili yao.

Akiongea na Malunde1 blog mganga mkuu wa wilaya ya Bukombe Dkt Honorata Rutatinisibwa amekiri kupokea miili ya askari wawili wa kike na kiume ambao ni WP 7106 PC Uria Mwandiga na askari namba G.2615 Pc Dustani Kimati.
 Askari waliojeruhiwa katika tukio hilo kuwa ni pamoja na mwenye namba E.5831 CPL David Ngupama Mwalugelwa aliyejeruhiwa kichwani na usoni na kwamba ameumizwa vibaya sehemu za midomo yake huku meno mawili yaking'oka na Mohamed Hassani Kilomo ambye amejeruhiwa kifuani na mguu wa kulia uliovunjika mfupa kwa kupigwa risasi.


Kwa mjibu wa Dr  Honoratha kutokana na hali za majeruhi kuwa mbaya wamewapa rufaa kwenda hospitali ya rufaa ya Bugando kwa matibabu zaidi.

Kamanda wa polisi mkoa wa Geita Joseph Konyo amethibitisha kutokea kwa tukio na kuahidi kutoa taarifa zaidi mara baada ya uchunguzi kukamilika.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527