Angalia Picha!! SHIRIKA LA AGPAHI LAFANYA WARSHA YA SIKU TATU KWA WAVIU WASHAURI MKOA WA SHINYANGA



Shirika la Kitanzania lisilo la kiserikali la Ariel Glaser Pediatric Aids Healthcare Initiative( AGPAHI) linalojihusisha na mapambano dhidi ya Virusi Vya Ukimwi (VVU) na UKIMWI katika halmashauri zote za mikoa ya Shinyanga,Simiyu pamoja na wilaya za Mbogwe na Bukombe kwa mkoa wa Geita, limefanya warsha ya siku tatu kwa watu wanaoishi na maambukizi ya Virusi vya Ukimwi wanaosaidia kuwaunganisha wateja na Vituo vya kutoa huduma za tiba na Matunzo kwa watu wanaoishi na VVU (CTC)-(WAVIU Washauri)




Warsha hiyo imefanyika kuanzia Machi 14-16,2016 katika Ukumbi wa Submarine Hotels mjini Kahama mkoani Shinyanga na kuhudhuriwa na WAVIU Washauri 30 kutoka katika halmashauri za wilaya 5 ambazo ni Kishapu,Msalala,Manispaa ya Shinyanga,Kahama Mji na Ushetu.

Lengo la warsha hiyo ni kuwajengea uwezo WAVIU Washauri ili waweze kuwaunganisha wateja kutoka kwenye jamii kwenda kwenye vituo vya tiba na matunzo na kuwafuatilia wateja waliopotea katika huduma na kuwarudisha pia kuainisha changamoto zinazosababisha wateja wasifike kwenye huduma na kutafuta njia sahihi za kutatua changamoto hizo.


Washiriki wa warsha hiyo pia walitembelea vituo vya tiba na matunzo (CTC),ambavyo ni Hospitali ya Mji wa Kahama na zanahati ya Ngogwa iliyopo katika kata ya Ngogwa halmashauri ya mji wa Kahama mkoani Shinyanga .Mwandishi mkuu wa Malunde1 blog,Kadama Malunde ametuletea picha 34 kuanzia mwanzo hadi mwisho wa warsha hiyo




Afisa Miradi Huduma Unganishi kwa jamii kutoka Shirika la AGPAHI, Cecilia Yona akifungua warsha ya WAVIU Washauri kutoka halmashauri za wilaya za mkoa wa Shinyanga,ambapo alisema shirika la AGPAHI limekuwa likitoa elimu ya VVU na UKIMWI kupitia watoa huduma ya elimu ya VVU na UKIMWI ngazi ya jamii ambao miongoni mwao ni WAVIU Washauri wanaofanya kazi zao katika vituo vya Tiba na Matunzo kwa watu wanaoishi na VVU.Alitumia fursa hiyo kuwataka WAVIU Washauri wanaojitolea kufuatilia wateja waliopotea katika tiba



WAVIU Washauri wakifuatilia kilichokuwa kinaendelea ukumbini,ambao walieleza kuridhishwa na shughuli zinazofanywa na shirika la AGPAHI katika kuwahudumia watanzania



Afisa Miradi Huduma Unganishi kwa jamii kutoka Shirika la AGPAHI, Cecilia Yona akielezea historia ya shirika la AGPAHI na namna linavyofanya kazi katika mikoa ya Shinyanga,Simiyu na Geita



WAVIU Washauri wakifuatilia kwa umakini moja ya mada zilizokuwa zinatolewa na wawezeshaji



Washiriki wa warsha hiyo wakifanya kazi ya vikundi kuhusu majukumu yao katika vituo vya kutolea tiba na matunzo



MVIU Mshauri Dakama Paschal kutoka CTC ya Ibadakuli katika manispaa ya Shinyanga akielezea majukumu ya Waviu washauri katika Vituo vya Kutolea tiba na matunzo



MVIU Mshauri Kanzaga Fabiani kutoka CTC ya Segese katika halmashauri ya wilaya ya Msalala mkoani Shinyanga akielezea changamoto wanazokutana nazo WAVIU washauri kuwa ni pamoja na wateja kutoa anuani za uongo kwa kudanganya majina na maeneo wanayoishi hali inayosababisha wateja kupotea katika tiba.



Mwezeshaji katika warsha hiyo Gladness Olotu ambaye ni muuguzi msaafu aliyebobea katika fani ya Ushauri nasaha akitoa elimu kwa washiriki wa warsha hiyo jinsi ya kumpa ushauri nasaha mteja.Gladness alisema umuhimu wa ushauri nasaha unamsaidia mteja kuwa na maamuzi sahihi ya kupima VVU.Alizitaja sifa za mnasihi kuwa ni lazima awe na elimu ya kutosha juu ya VVU na UKIMWI,awe mkarimu,msiri,anayejiamini na azingatie muda



Mviu mshauri Rose Kosuli kutoka CTC ya Kambarage katika manispaa ya Shinyanga akieleza maana ya ushauri nasaha kwa niaba ya kundi lake



Washiriki wa warsha hiyo wakionesha igizo jinsi huduma za ushauri zinavyofanyika katika vituo vya tiba na matunzo.Katika igizo hilo mtaalam wa ushauri nasaha anatumia lugha mbaya katika kuhudumia wateja,jambo ambalo halitakiwi kufanywa na mnasihi pale mteja anapohitaji huduma ya ushauri



Igizo la pili kuhusu Ushauri nasaha..Pichani kushoto ni mwezeshaji katika warsha hiyo Flora Selutongwe akionesha igizo na Kanzaga Fabian jinsi mteja anavyotakiwa kuhudumiwa vizuri anapohitaji huduma hiyo



Mwezeshaji katika warsha hiyo Gladness Olotu akitoa elimu ya ushauri nasaha na upimaji wa VVU,ambapo aliwataka wanasihi kutoa ushauri nasaha katika chumba chenye usiri,nafasi ya kutosha,kisiwe na mwingiliano wa watu,kuwe na hewa ya kutosha,viti viwili, meza,kitabu cha usajiri na fomu za rufaa



Mwezeshaji katika warsha hiyo Flora Selutongwe ambaye ni muuguzi katika hospitali ya mji wa Kahama akitoa elimu ya lishe na utapiamlo kwa washiriki wa warsha hiyo.Selutonge pia alielezea mkakati wa taifa wa kudhibiti Ukimwi huku elimu yake ikijikita zaidi juu ya uhusiano wa Kifua kikuu na Ukimwi,kuzuia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto,matumizi sahihi ya kondomu na matumizi sahihi ya dawa za kupunguza makali ya VVU



Washiriki wa Warsha hiyo wakiwa katika hospitali ya mji wa Kahama kwa ajili ya kutembelea kituo cha tiba na matunzo kwa watu wanaoishi na VVU.Kulia ni Flora Selutongwe ambaye ni muuguzi katika hospitali ya mji wa Kahama akiwa na Afisa Miradi Huduma Unganishi kwa jamii kutoka Shirika la AGPAHI, Cecilia Yona.

Lengo la kutembelea CTC hiyo ni WAVIU Washauri kujifunza namna ya utoaji wa elimu,mbinu za ufuatiliaji wa watoro na jinsi ya kuunganisha huduma ya RCH na CTC



Kushoto ni muuguzi katika hospitali ya mji wa Kahama Flora Selutongwe akisikiliza neno kutoka kwa Afisa Miradi Huduma Unganishi kwa jamii kutoka Shirika la AGPAHI, Cecilia Yona wakielekea katika CTC ya hospitali ya mji wa Kahama



Hapa ni katika CTC ya hospitali ya mji wa Kahama,kulia ni Afisa tabibu katika hospitali ya mji wa Kahama Flora Mwinuka anayefanya kazi katika kitengo cha CTC akieleza namna walivyofanikiwa kuanzisha vikundi vya watoto na watu wazima katika kituo hicho walioko kwenye huduma ya tiba na matunzo ambao pia hupewa elimu ya VVU na UKIMWI na kuwajengea uwezo wa kutoa elimu kwa wengine katika jamii


Tunafuatilia kinachoendelea ......



Wa kwanza kushoto (nyuma) ni bi Debora Mpagama ambaye ni Mtangazaji wa Radio Free Africa kipindi cha UKIMWI NA JAMII kila siku ya Jumamosi saa 5:15 asubuhi mpaka saa 6:00 mchana ,akifuatiwa na bi Amina Mbwambo ambaye ni mtangazaji wa kipindi cha AFYA kichorushwa Radio Kahama kila siku ya Jumamosi saa 6:00 mchana hadi saa 7:00 mchana wakifuatilia kilichokuwa kinaendelea katika CTC ya hospitali ya mji wa Kahama



Afisa tabibu katika hospitali ya mji wa Kahama Flora Mwinuka anayefanya kazi katika kitengo cha CTC akionesha kadi anayotakiwa kuwa nayo mteja aliye katika huduma za tiba na matunzo



Tunamsikiliza Afisa tabibu katika hospitali ya mji wa Kahama Flora Mwinuka



Watoa huduma katika CTC ya hospitali ya mji wa Kahama wakiwa katika chumba cha dawa kwa ajili ya watu wanaoishi na VVU


Washiriki katika warsha hiyo wakitoka kwenya chumba cha Ushauri nasaha na Upimaji wa damu kwa hiari(VCT) katika CTC ya hospitali ya mji wa Kahama



Hapa ni katika Zahanati ya Ngogwa iliyopo katika halmashauri ya mji wa Kahama ambapo pia kuna kituo cha CTC.Washiriki wa warsha hiyo pia walipata fursa ya kujifunza mambo mbalimbali juu ya VVU na Ukimwi pamoja na changamoto mbalimbali wanazokutana nazo WAVIU washauri wakati wa kuhudumia wateja.



Majengo ya Zahanati ya Ngogwa katika halmashauri ya mji wa Kahama.Zahanati hii ilijengwa mwaka 1947,mpaka sasa ina majengo hayo matatu madogo yanayoonekana pichani.Wagonjwa wanaofika hapo ni wengi lakini changamoto kubwa ni upungufu wa majengo.



Haya ni majengo ya zahanati ya Ngogwa yamefanyiwa ukarabati na shirika la AGPAHI kwa ajili ya kutumika kutolea huduma ya tiba na matunzo




Washiriki wa warsha hiyo wakiwa katika chumba cha mapokezi zahanati ya Ngogwa ,wakijifunza namna wateja wanavyopokelewa na kuanzishiwa huduma katika kituo hicho



Mganga mfawidhi katika zahanati ya Ngogwa, Flora Sanga akizungumza na WAVIU washauri waliotembelea kituo hicho.Sanga alisema maambukizi ya VVU katika eneo la Ngogwa na maeneo jirani ni makubwa kutokana na jamii kukosa elimu ya VVU na UKIMWI pamoja na mila na desturi zilizopo katika jamii ikiwemo ndoa za mitaala na wanajamii kufanya ngono na mtu aliyefiwa na mke au mme bila kufuatilia chanzo cha kifo cha mtu huyo.



Mganga mfawidhi katika zahanati ya Ngogwa Flora Sanga akizungumza na WAVIU washauri ambapo alitumia fursa hiyo kuiomba jamii kuwa na tabia ya kupima afya mara kwa mara ili pale inapobainika wamepata maambukizi ya VVU basi waanze tiba mara moja



WAVIU Washauri wakifuatilia kilichokuwa kinaendela katika CTC ya Ngogwa iliyopo katika halmashauri ya Mji wa Kahama


Kushoto ni Afisa Miradi Huduma Unganishi kwa jamii kutoka Shirika la AGPAHI, Cecilia Yona akiwahamasisha WAVIU washauri kutumia vyema elimu waliyopewa na shirika la AGPAHI



Afisa Miradi Huduma Unganishi kwa jamii kutoka Shirika la AGPAHI, Cecilia Yona aliwaasa watu waliopata maambukizi ya VVU kufuata masharti waliyopewa na wataalam ikiwemo kuhakikisha wanatumia dawa za kufubaza makali ya VVU.Afisa huyo pia alisisitiza umuhimu wa CTC kuunda vikundi vya WAVIU,watoto na akina mama.



Washiriki wa warsha hiyo wakiwa katika picha ya pamoja na wawezeshaji katika warsha hiyo iliyodumu kwa muda wa siku tatu mjini Kahama



Washiriki wa warsha hiyo wakiwa katika picha ya pamoja na wawezeshaji katika warsha hiyo iliyodumu kwa muda wa siku tatu mjini Kahama

Picha zote na Kadama Malunde- Malunde1 blog

BONYEZA HAPA KUONA PICHA ZA WARSHA YA WAVIU WASHAURI MKOA WA SIMIYU 

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527