MUME ACHINJA MKE WAKE KAMA KUKU,KISA " KAPATA WAPI PESA YA SALUNI"


HII ni zaidi ya ukatili! Jiji la Tanga bado linazizima kufuatia mauaji ya kutisha yanayodaiwa kufanywa na mwanaume aitwaye Khalfan  Hamad (46), dhidi ya mkewe, Mary Lucas (20) kwa kumchinja na panga kisa kikidaiwa ni wivu wa mapenzi.


Tukio hilo lililoacha simulizi ya kushangaza miongoni mwa wanandoa na wanaotarajia kuingia, lilijiri Aprili 18, mwaka huu nyumbani kwa mwanaume huyo, Mtaa wa Mapinduzi ‘A’ Kata ya Duga jijini hapa.

WANACHOKIJUA POLISI WA TANGA

Kamanda wa Polisi Mkoa  wa Tanga, ACP Zuberi Mwombeki alitangaza kwa waandishi wa habari kwamba, mauaji hayo yalitokea saa nne na nusu asubuhi ya Aprili 18 mwaka huu.

Alisema chanzo cha tukio hilo ni wivu wa kimapenzi kati ya wawili hao  ambapo marehemu alimuomba mumewe pesa kiasi cha shilingi elfu kumi aende saluni kutengeneza nywele lakini mwanaume akasema hana.

“Mwanaume hakumpa pesa marehemu lakini baadaye alimkuta amesuka na ndipo ugomvi ulipoanzia hapo hadi kutokea mauaji hayo,” alieleza kamanda huyo.

MAJIRANI WANASEMAJE?

“Jamani sisi wenyewe tumeshtuka sana kwa kifo cha Mary, mimi nimeongea naye akiwa anakwenda saluni na hata aliporudi. Kama angejua ndiyo siku yake ya kufa naamini asingekwenda. Inauma sana!


“Mary alitoka saluni akiwa amependeza maana alitengenezwa nywele vizuri sana. Mimi mwenyewe nilimsifia. Kufika nyumbani kwake, mzozo ukaanza.

“Mumewe alitaka kujua alikotoa shilingi elfu kumi ya kuendea saluni maana yeye hakumpa. Mzozo ulikwenda hadi mwanaume akachukua panga na kumchinja. Naamini ni wivu,” alisema jirani mmoja.

 KUMBE WALIKUWA NA HISTORIA YA UGOMVI

Jirani mwingine, Shaban Juma yeye alisema: “Hawa watu wameishi katika hali ya kutoelewana na walikuwa wakigombana kila wakati, lakini hatukujua kama litatokea hili kwani mara zote katika kugombana kwao, mwanaume ndiye aliyekuwa akipigwa jambo ambalo liliwafanya watu wa karibu yake kumshauri  kuvunja uhusiano wao kulikoni aibu ya kupigwa na mke.”

Jennifer   Charles yeye pia ni jirani, alisema: “Siku ya tukio Mary alimwomba mumewe hela ya kwenda kutengeneza nywele saluni  lakini mume hakuwa na pesa siku hiyo lakini baada ya kuondoka nyumbani,  marehemu naye alikwenda saluni.

“Baadaye mume aliporudi  nyumbani hakumkuta  Mary lakini mara alirudi akiwa ametengenezwa nywele jambo lililomfanya  bwana  kuhisi kuwa fedha hizo amehongwa na mwanaume  mwingine  tofauti na  yeye na hivyo kuzuka ugomvi  huo.”

 MUME ALITOKA NJE AKITAMBA KUUA

Baada ya Jennifer kumaliza kusimulia hayo, Juma  Ally, naye ni jirani, akaendeleza: “Hatukujua kilichoendelea katika mzozo wao, lakini baadaye ukimya ulitawala. Muda mfupi mbele mume alitoka nje na kutuambia kwamba ameshaua  huko ndani  kwani amechoka kupigwa na sasa amejibu mapigo.

“Kwanza tulijua anatutania lakini  tulivyoona kimya kimezidi tukaamua kuingia ndipo

tulipomkuta marehemu akiwa chini, akitoka damu nyingi. Tuliogopa kwa kweli. Mary mrembo tunayemjua sisi, amelala chini na damu chapachapa.

“Alikuwa ana majeraha  makubwa sehemu ya shingo na kichwani  yaliyotokana na kupigwa na panga. Ilionekana panga lilikuwa kali sana na panga lenyewe lilikuwa pembeni yake. Ndipo tulipoamua kumkimbiza Hospitali ya Mkoa, Bombo ambapo alipoteza maisha wakati madaktari wakihangaika kuokoa uhai wake.”

ASINGEKUFA MKE

Naye, Fatuma Ramadhani alisema kutokana na ugomvi wa mara kwa mara kati ya wawili hao na mwanaume kupigwa kila wakati, majirani waliamini siku moja mume  huyo ndiye angekuja kupata madhara hata kufa kutokana na alivyokuwa akipigwa.

MTUHUMIWA KUPANDA MAHAKAMANI WAKATI WOWOTE

Kamanda Mwombeki alisema upelelezi unaendelea ili kuweza kumfikisha mahakamani mtuhumiwa huyo.

Marehemu Mary alizikwa katika eneo la Mwakizaro jijini Tanga, siku ya pili baada ya tukio hilo la kuhuzunisha.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527