Watu
wanaosadikiwa kuwa ni majambazi wamebomoa kaburi la Napegwa Kishaluli
(75) mkazi wa Mailimoja Kibaha mkoani Pwani aliyezikwa Aprili 20 mwaka
huu na kumvua nguo zote pamoja na kuchukua mikoba aliyokuwa amezikwa
nayo.
Tukio
hilo lilitokea Aprili 24 mwaka huu katika Kata ya Tangini jirani na
soko la Loliondo ambako baada ya mazishi kaburi hilo liliwekewa mlinzi
kwa muda wa wiki moja.
Mkataba wa mlinzi huyo ulipomalizika aliondoka na siku iliyofuata kaburi hilo lilivunjwa.
Watu
wa karibu na familia ya marehemu wamesema kuwa baada ya mazishi
ulikuwapo uvumi kwamba marehemu alizikwa na vitu vya thamani zikiwamo
fedha, simu, pete na mikufu ya dhahabu pamoja na nguo zenye thamani
kubwa.
Hata
hivyo, taarifa zinasema marehemu Kishaluli alizikwa na mikoba miwili ya
nguo na vitu vyake vingine na kwamba kabla ya kifo chake aliagiza
azikwe na vitu vyake.
Akizungumza
na Mwandishi wetu jana,ndugu wa marehemu,Bartholomew Mwanjile alisema
baada kuzika walilazimika kuajiri mtu wa kulinda kaburi hilo la ndugu
yao kwa wiki moja lakini siku moja baada ya mkataba kumalizika kaburi
hilo lilivunjwa.
“Tuliweka mlinzi alinde kaburi hilo kwa wiki moja tukiamini litakuwa limekauka kwa sababu lilitengenezwa kwa zege.
“Tuliamini
watu wenye nia mbaya watashindwa kulivunja jambo ambalo limekuwa
kinyume kwa vile baada ya muda huo kumalizika kaburi lilibomolewa na
watu wasiojulikana ambao waliamini ndani ya mikoba hiyo kulikuwa na
fedha,” alisema Mwanjile.
Mwanjile
alisema baada ya kuvunja kaburi hilo majambazi walifungua jeneza na
kupekua ndani kwa kuligeuza na kuliweka tofauti na lilivyokuwa awali,
baada ya kumvua marehemu nguo zote na viatu alivyokua amevalishwa na
hata soksi nazo walichukua.
Alisema
tukio la kuvunjwa kwa kaburi hilo limetokea baada ya uvumi kuwa ndugu
yao alizikwa na nguo na vitu vingine zikiwamo fedha, kiasi cha Sh
milioni 8, cheni ya dhahabu,simu za gharama na kompyuta
mpakato(laptop),jambo ambalo si la kweli.
“Tulimzika
ndugu yetu na mikoba ya nguo zake ambazo aliagiza kabla ya mauti
kumkuta na kaburi tulijenga kwa zege lakini tukashauriana tuweke mlinzi,
hapo ndipo watu wakaanza kutia shaka wakadhani kuna vitu vya gharama
jambo ambalo si kweli,” alisema Mwanjile.
Kamanda
wa Polisi Mkoa wa Pwani, Jafari Mohamedi alithibitisha kutokea kwa
tukio hilo na kwamba uchunguzi unaendelea na watakaobainika
watachukuliwa hatua za sheria.