KILICHOSEMWA NA CHADEMA KUHUSU MUDA WA KUJIANDIKISHA KWENYE DAFTARI LA KUDUMU LA MPIGA KURA KUPITIA BVR

Chama cha demokrasia na maendeleo (Chadema) kimesema muda wa mwezi mmoja uliotolewa na tume ya taifa ya uchaguzi ( NEC ) hautoshi kuandikisha wananchi zaidi ya milioni 24 katika daftari la kudumu la mpiga kura kwa kutumia mfumo mpya wa Biometric Votres Registration ( BVR ), badala yake wameitaka serikali kuongeza muda wa miezi minne zaidi.


Mwenyekiti wa chama hicho Mh. Freeman Mbowe, akihutubia maelfu ya wakazi wa Mwanza na mikoa jirani ya kanda ya ziwa katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa Furahisha jijini Mwanza, amesema muda wa siku 30 uliotolewa na tume hiyo kwa ajili ya kuandikisha wapiga kura hautoshi kutokana na tume kutokuwa na vifaa vya kutosha na pia ikizingatiwa kuwa mtu mmoja anatumia dakika 5 hadi 10 kuandikishwa kwenye daftari hilo.

Kwa upande wake naibu katibu mkuu wa Chadema – Zanzibar, Salum Mwalimu amesema uamuzi wa Chama cha mapinduzi kuwapa onyo baadhi ya wanachama wake, wakiwemo wajumbe wa kamati kuu ambao wametangaza mapema nia ya kugombea nafasi ya urais, itakayoachwa wazi na rais Jakaya Kikwete baada ya uchaguzi mkuu baadaye mwaka huu ni ishara na dalili za wazi kwamba chama hicho hakijajiandaa kisaikolojia kuwa chama cha upinzani kutokana na nguvu kubwa inayoonyeshwa na Chadema pamoja na Ukawa.

Wakizungumza katika mkutano huo mkubwa, baadhi ya wabunge wanaotokana na chama cha demokrasia na maendeleo akiwemo mbunge wa Arusha mjini Mh. Godbless Lema pamoja na mwenyekiti wa taifa wa baraza la vijana wa Chadema ( Bavicha ), Patrobas Katambi wamewataka watanzania kupigania nchi yao kwa mambo ya msingi bila uwoga ili rasilimali zilizopo ziweze kuwanufaisha wananchi wote.
Via>>Itv

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527