ASKARI MAGEREZA NA ASKARI WA FFU WAKAMATWA NA NOTI BANDIA MILIONI 1 NA SARE ZA JWTZ HUKO SIMIYU

Naibu kamishna wa jeshi la polisi Mkoani Simiyu Charles Mkumbo akiwaonyesha waandishi wa habari (hawapo pichani) baadhi ya sare za JWTZ ambazo zilikamatwa askari wa jeshi la polisi Mkoani Simiyu pamoja na Askari Magereza wilayani Bariadi

Baadhi ya noti bandia walizokutwa nazo


Naibu kamishna wa jeshi la polisi Mkoani Simiyu Charles Mkumbo akiwaonyesha waandishi wa habari (hawapo pichani) baadhi ya pesa bandia ambazo zilikamatwa askari wa jeshi la polisi


Sare zilizokamatwa.

Jeshi la polisi mkoani Simiyu linawashikilia askari wawili wa jeshi la magereza na polisi kwa kukutwa na noti bandia ikiwa ni pamoja na sare za jeshi la wananchi Tanzania (JWTZ).
Akitoa taarifa za kukamatwa kwa askari hao Naibu Kamishna wa jeshi la polisi Mkoani Simiyu Charles Mkumbo alisema kuwa askari hao walikamatwa juzi majira ya saa 9 mchana katika mtaa wa Old Maswa kata ya Nyakabindi Wilayani Bariadi.
Alisema askari hao walifika kwenye kibanda cha M-pesa kinachomilikiwa na Mwalimu wa Shule ya sekondari Old Maswa Kassian Luhende (29), wakiwa na pikipiki yenye namba za usajili T-403 CXW aina ya Sunlg kwa lengo la kuweka fedha hizo kweye simu.
Alisema baada ya Mwalimu huyo kupokea fedha kiasi cha noti 10 zenye thamani ya Shilingi 10,000 alizitilia shaka ambapo alipoendelea kuzikagua zaidi alizigundua kuwa siyo fedha halali.
Mkumbo alieleza kuwa Mwalimu huyo baada ya kugundua fedha hizo kuwa ni feki, alichukua jukumu la kuwajulisha majirani zake ili kuomba Msaada wa kuweza kuwakamata askari hao baada ya kugundua siyo watu wema.
Aidha alieleza kuwa baada ya mwalimu kutoa taarifa kwa majirani, wananchi walikusanyika na kuanza kuwahoji askari hao, ndipo askari mmoja alipotoa kitambulisho kuwa yeye ni askari na mwingine kujitambulisha kuwa ni dereva bodaboda.
Alibainsiha kuwa wananchi baada ya kuambiwa hivyo waliwatilia shaka zaidi ambapo walitoa taarifa Kituo cha polisi Bariadi, na askari kwenda kuwakamata.
Mkumbo aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni askari mwenye namba H 2420 PC Seleman Juma (25) ambaye ni askari wa kikosi cha kutuliza gasia FFU Mkoani Simiyu, na askari namba B.6499 WDR Edmund Masaga (28) ambaye ni askari Magereza wilayani Bariadi.
Kamanda Mkubo alieleza kuwa baada ya askari hao kukamatwa mmoja wao PC Selemani Juma alipopekuliwa katika mfuko wa suruali yake alikutwa na noti zingine za Bandia za elfu kumi kumi na jumla yake kama zingelikuwa halali zingelikuwa na thamani ya Shilingi 1,920,000.
Mbali na hilo Mkumbo alieleza kuwa Askari huyo alipokwenda kupekuliwa nyumbani kwake alikutwa na sare za JWTZ ambazo ni Pensi 4, T-shirt 2, Kombati 1 pamoja na Kitambaa.
Hata hivyo Mkuu huyo wa polisi alieleza kuwa uchunguzi zaidi unaendelea ili kubaini mtandao mzima wa usambazaji wa noti bandia ndani ya mkoa huo, huku akieleza kuwa mara baada ya uchunguzi kukamilika askari hao watachuliwa hatua za kinidhamu pamoja na kisheria.
Alitoa onyo kwa askari Mkoani Simiyu kuacha tamaa ya pesa na badala yake waridhike na ajira zao zinazowapatia pesa halali, huku akieleza kuwa kwa atakayebainika atachukuliwa hatua kali za kisheraia na nidhamu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527