Hakimu mkazi mwandamizi mfawidhi wa mahakama ya mkoa
wa Shinyanga John Chaba akizugumza leo wakati wa maadhimisho ya siku ya sheria nchini,ambapo kimkoa yamefanyika katika viwanja vya mahakama ya hakimu mkazi Shinyanga leo asubuhi-picha na Kadama Malunde
Ifuatayo ni hotuba iliyotolewa na hakimu huyo
Mhe. Mkuu wa Wilaya (ambaye kimsingi unamwakilisha Mkuu
wa (M) wetu wa Shy)
Mhe.
Hakimu Mkazi
Mfawidhi (W) Shinyanga,
Wahe. Mahakimu wa ngazi zote,
Mhe. Wakili wa Serikali Mfawidhi,
Shinyanga,
Mhe. Mwenyekiti wa Chama cha Mawakili
wa Kujitegemea Tawi la (M) Shinyanga,
Wahe. Mawakili wote wa Serikali na
Mawakili Binafsi/Kujitegemea,
Mhe. Mtendaji wa Mahakama
(M) wa Shinyanga,
Wahe. Makamanda wa vyombo vya Ulinzi,
Magereza, na Usalama wa Mkoa,
Wahe. Viongozi wa Dini kutoka Mathehebu
mbalimbali,
Wahe: Viongozi na Wakuu
wa Taasisi za Serikali mliopo, Mashirika ya Umma, na Viongozi wote wa Vyama vya Siasa,
Watumishi wote wa Mahakama wa ngazi zote mliopo hapa,
Wageni
waalikwa, Mabibi na Mabwana. (Itifaki imezingatiwa)
Bwana
Yesu asifiwe, Tumsifu Yesu Kristo, Asalaam Aleikhum,
UTANGULIZI
Mhe. Mgeni Rasmi na Wageni Waalikwa, kwa
heshima kubwa kabisa naomba nianze kwa kuwatakia Kheri ya Mwaka Mpya – 2015.
Pili,
naomba nitumie fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutupa afya njema
na rehema kuiona siku hii njema. Lakini pia, naomba nikushukuru sana wewe Mhe.
Mgeni Rasmi na Wote mlioalikwa kwa kukubali mwaliko wetu ili kujumuika nasi
kwenye maadhimisho haya ya siku ya Sheria hapa Nchini (Law Day) ambayo kimsingi
huadhimishwa kila mwaka. Hakika ni furaha kubwa kuwa pamoja nanyi katika
kuadhimisha na kusherehekea maadhimisho haya kama wadau muhimu wa chombo hiki
cha Mahakama.
Aidha, natambua na kuthamini kazi na majukumu
mazito mliyonayo katika jamii yetu na Taifa kwa ujumla. Hata hivyo, siku hii
njema mmeipa umuhimu wa pekee na kuonyesha ishara ya upendo, mshikamano,
ushirikiano na udugu kama watanzania wamoja na wenye nia moja ya kulijenga
Taifa lenye nguvu. Hali hii inaonyesha kwamba hakika mnathamini na kutambua
vema kazi na wajibu wa chombo hiki katika jamii yetu.
Mhe. Mgeni Rasmi na Wageni Waalikwa, leo
hii sisi tuko hapa Mkoani Shinyanga, na kuna wenzetu ambao wako maeneo mengine
Nchini kote wakiadhimisha siku hii muhimu na adhimu. Kama tunavyofahamu, siku
hii ya Sheria Nchini ni siku ambayo inaashiria mwanzo rasmi wa Kalenda ya
kuanza kwa shughuli za Mahakama Nchi nzima. Kwa kawaida, siku hii hutumika
kuwaombea dua pamoja na sala watumishi wote wa Mahakama
hususani watendaji wakuu wakiwemo Wahe. Majaji na Mahakimu ili waweze kufanya
kazi zao katika misingi ya haki, lakini zaidi wakimtumainia Mungu kwa kuwa
tunaamini kwamba watendaji hawa kwa ujumla wanahitaji kuwa na hofu ya Mwenyezi-Mungu
ili waweze kufanya kazi zao za utendaji wa haki kwa wananchi na Taifa kwa
ujumla kwa mujibu wa Sheria.
Kwa niaba
ya Mahakama ya Mkoa – Shinyanga, napenda kuwaalika tena leo hii katika
maadhimisho haya na kuwashukuruni nyote kwa kufika kwenu, hususani viongozi
wetu wa dini ambao kimsingi wamefanya kazi kubwa kutuombea sisi watendaji na
watumishi wengine ili tuendelee kuwa na afya njema, hekima, busara na uwezo
tupate kutekeleza majukumu yetu kwa mujibu wa kanuni, taratibu na Sheria za
Nchi.
MADHUMUNI
Mhe.
Mgeni Rasmi na Wageni waalikwa,
siku hii ya leo ni siku muhimu sana kwetu sote. Umuhimu wake haupo tu kwa
Mahakama pekee bali hata kwa wadau wa Mahakama kwa ujumla. Kwa
pamoja tunapata wasaa mzuri
wa kukumbushana wajibu wetu na pia kujikosoa na kukubali kukosolewa lakini
tukiwa na dhamira moja tu ya kuhakikisha kwamba tunafanya kazi kwa mujibu wa
kanuni, taratibu na sheria za Nchi. Kwa wale wenye uelewa wa sheria
mtakubaliana na mimi kuwa moja ya msingi mkuu wa haki unasema - sio tu kwamba haki itendeke, lakini ionekane kuwa
imetendeka.
Mhe. Mgeni Rasmi,
kama ilivyo ada, Siku ya Sheria Nchini huadhimishwa ikiwa na kauli mbiu. Kwa
mwaka huu, kauli mbiu inasema; “FURSA YA KUPATA HAKI : WAJIBU WA
SERIKALI, MAHAKAMA NA WADAU”.
Mhe. Mgeni Rasmi na Wageni Waalikwa,
naomba nijadili kauli mbiu hii kwa ufupi. Unapoisoma kauli mbiu ya mwaka huu kuna
mambo mawili muhimu yanayohitaji kujadiliwa. Mambo haya nimeyaweka katika mfumo
wa maswali ili niweze kueleweka vizuri.
Moja,
tunaposema fursa ya kupata haki hii ina maana gani katika mchakato mzima wa
utoaji haki hapa Nchini? na lingine ni nini wajibu
wa Serikali, Mahakama na Wadau kwa ujumla katika mchakato huu wa utoaji haki?.
I.
MAANA YA NENO HAKI
Kimsingi neno Haki lina maana pana na halina
tafsiri ya moja kwa moja. Kwa tafsiri ya
Kikamusi, kwa mujibu wa kamusi ya Oxford neno haki (Justice)
linatafsiriwa kuwa ni “hali ya usawa na busara” (The guality of being fair and reasonable).
Pia, Kamusi ya Black’s
Law imetafsiri neno haki kuwa ni “Kulinda ukweli na kuadhibu mabaya kwa
kutumia usawa”, yaani “Protecting
Rights and punishing wrongs using fairness)
Na kwa upande, Shirika la Maendeleo la Umoja wa
Mataifa (UNDP) kwenye moja ya repoti
yake ya tarehe 09/03/2004 imetafsiri dhana hii ya Fursa ya Kupata haki kuwa ni
sehemu ya uzima au uhai wa Shirika hili la Maendeleo la Umoja wa Mataifa ambalo
limepewa mamlaka ya kupunguza/kushusha kiwango cha umaskini na kukuza utawala
wa Kidemokrasia miongoni mwa jamii ya Kimataifa.
I.
FURSA YA KUPATA HAKI.
Mhe. Mgeni Rasmi na Wageni waalikwa, fursa yakupata Haki ni dhana pana ambayo
msingi wake ni uwezo wa watu kutafuta na kupata haki stahiki kutoka Taasisi
rasmi na zisizo rasmi za utoaji haki kwa kuzingatia usawa na vigezo vya haki za
Binadamu. Fursa hii ya kupata haki
inaweza kuelezewa vizuri zaidi kwa mtazamo wa wazo la kisiasa lijulikanalo kama
egalitariarism ikiwa na maana
ya believing
in or based on the principle that all people are equal and deserve aqual rights
and opportunities (kwa lugha ya kitaalamu). Dhana hii, ni mfululizo wa falsafa ya kisiasa
unaolenga usawa wa mtu mmoja mmoja. Kila mtu anapaswa kuwa sawa na mwengine, aangaliwe
sawa, au kwa uwiano ulio sawa. Kwa mafano, Katiba ya Nchi na Sheria nyingine zieleze
wazi kuwa msimamo wa utawala wa sheria usiwe tu katika kusimamia haki za msingi
kwa wananchi, bali iwe kwa ajili ya kusimamia usawa na heshima kwa watu wote.
Falsafa hii inapigania zaidi uwepo wa usawa wa thamani ya mtu pamoja na utu
wake. Ni dhana inayofungamana na mfumo wa kisiasa na kijamii na kimsingi dhana
hii inashadidia zaidi ufanisi wa upatikanaji wa haki uliojikita katika misingi
ya usawa.
Kwa ustaarabu huo, fursa ya kupata haki haitazami/kuangalia tofauti
za kiuchumi au kijamii zilizopo kati ya mtu na mtu. Dhana iliyo sawa na hii
imerithiwa na Katiba yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayosimamia,
mbali na mambo mengine, upatikanaji wa haki. Hili limebainishwa wazi na Ibara ya 13 ya Katiba; ambayo inasema:-
“Watu
wote ni sawa mbele ya sheria, na wanayo haki, bila ya ubaguzi wowote kulindwa
na kupata haki sawa mbele ya sheria”
Mhe.
Mgeni Rasmi na Wageni Waalikwa, tujikumbushe kidogo kauli
iliyotolewa na Wah. Majaji wa Mahakama ya Rufaa ya Tanzania, JJ.A Omar, Ramadan
na Mnzavas iliyotolewa katika kesi ya Clay Laway Vs. Republic
(1992) CA T.L.R. 72 walisema:-
“All individuals should be free
and equal in considering that every person is entitled to recognition and
respect of his dignity, therefore they entitle equality before the law without
any discrimination towards access to justice and right to life in particular.”
Mhe. Mgeni Rasmi na Wageni Waalikwa,
Kama ilivyobainishwa na Mahakama ya Rufaa, fursa ya kupata haki inamuwezesha
kila mmoja wetu kuitumia sheria kwa minajili ya kulinda haki zetu. Hata hivyo,
hili litawezekana pale tu vyombo vya umma pamoja na mfumo wa utoaji haki na
taasisi husika utapohakikisha kuwa kila mtu analindwa na sheria na anauwezo wa
kuufikia mfumo waa utoaji haki. Tukiwa tumejumuika hapa, tunapaswa kukumbuka
kuwa, miongoni mwa mambo yanayoleta usawa katika nchi ni fursa sawa ya kupata
haki (rights), uwepo wa uhuru wa mtu binafsi,
na fursa ya kupata haki yenyewe (justice). Tukumbuke kwamba, dhana hii ya fursa ya kupata haki imejikita katika
sifa kuu moja, kwamba hawa watunga sheria pamoja na maafisa wa juu wa Serikali
wawe watenda haki (fair and just) katika
mchakato mzima wa utoaji/upatikanaji wa haki kwa watu wote.
Kwa maana hiyo, ikitokea
kuwepo kwa ukiritimba, ugumu au ukaidi wa makusudi wa kutotenda haki, Mahakama
ndicho chombo pekee kilichopewa mamlaka ya juu ya kusimamia haki ya kila mmoja
wetu. Wakati Ibara ya 107A ya Katiba inasema:
“Mamlaka yenye kauli ya mwisho ya utoaji haki katika
Jamhuri ya Muungano itakuwa ni Mahakama”.
Ibara ya 13 (3) ya Katiba yenyewe
inasema:-
“Haki
za raia, wajibu na maslahi ya kila mtu na jumuiya ya watu yatalindwa na
kuamuliwa na Mahakama na vyombo vinginevyo vya Mamlaka ya Nchi vilivyowekwa na
sheria au kwa mujibu wa sheria”.
Hii ina-maana kwamba Mahakama kama chombo pekee
chenye mamlaka ya mwisho ya utoaji haki hapa Nchini, endapo haki inayotafutwa
katika vyombo vingine vya Kisheria itashindikana kupatikana, jibu lake ni
Mahakama zetu. Hata hivyo, tunaweza kusema, iwapo fursa ya kupata haki
itatolewa katika Taasisi zote za Serikali na zisizo za Serikali pamoja na wadau
wengine kwa ufasaha, Mahakama zetu hazitakuwa na mlundikano wa maashauri au kesi
kutokana na migogoro mbalimbali katika jamii yetu.
Mhe. Mgeni rasmi na Wageni waalikwa, sambamba
na yale niliyoyasema hapo awali, kuna mahusiano ya moja kwa moja kati ya
uelewa, kuwa na habari muhimu ama ufahamu wa namna ambavyo Mahakama inafanya
shughuli zake kwa ujumla. Kimsingi, wananchi wanayohaki ya kufahamu shughuli za
Mahakama siyo tu katika kutafsiri sheria na kutoa haki, bali pia kutambua
sheria husika ambazo mara nyingi hutumika Mahakamani. Kwa mfano; Wananchi wanahaki
ya kujua sheria za Makosa ya Jinai na Madai, migogoro ya ardhi, Mambo ya
Mirathi, Sheria za Uchaguzi, Sheria za Mazingira, Sheria zinazohusu mali-asili
(nishati na madini, utalii), vyombo vya habari, n.k.
Hata hivyo,
haitoshi kwa huyu mwananchi kuwa na uelewa, kupata habari muhimu na kufahamu
namna ambavyo Mahakama inafanya shughuli zake kwa ujumla. Kubwa zaidi ni kwa mwananchi huyu kuipata fursa ya kupata haki
yake, na kwa upande wa pili, ni namna gani Serikali, Mahakama yenyewe na Wadau
kwa ujumla wanawajibika ipasavyo kuhakikisha kwamba mwananchi huyu anapata
fursa hii kwa mujibu wa sheria na bila kikwazo chochote. Napenda kutumia fursa hii kuwaomba na kuwakumbusha wale wote ambao
tumepewa dhamana ya kushughulikia upatikanaji na utoaji wa haki kwa wananchi tunatimiza
wajibu wetu ipasavyo.
Kwa maoni yangu,
ili ufahamu huu umfikie mwananchi hatuna budi kushirikiana kwa pamoja
kuwaelimisha wananchi na jamiii kwa ujumla kuitumia fursa hii ya kupata haki
katika vyombo vinavyohusika kama moja ya hatua za msingi katika kuufikia
mfumo wa utoaji haki na utatuzi wa migogoro katika jamii yetu kwa ujumla.
Pamoja na ukweli kuwa Mahakama ndicho chombo pekee chenye
mamlaka ya kutoa haki kwa wananchi, kwa
upande mwingine, Serikali na Wadau wote wa Mahakama wameendelea kuwa kiungo
na sehemu muhimu siyo tu katika kuhakikisha fursa ya kupata haki inafikiwa, lakini pia, wamekuwa na wajibu wa
kuhakikisha kwamba fursa hii inafikiwa tena kwa wakati. Hii ina-maana kwamba endapo chombo kimoja
kitashindwa kutekeleza wajibu wake ipasavyo inaweza kuwa kikwazo kwa fursa hiyo
kufikiwa kwenye chombo kingine, jambo
ambalo kwa maoni yangu ni hatari na linaweza kupelekea haki kuchelewa
kupatikana ama kutopatikana kabisa. Tukumbuke kwamba ufanisi wa chombo
kimoja cha utoaji wa haki unategemea sana utendaji wa chombo kingine katika
mchakato mzima wa utoaji haki hapa nchini.
II.
WAJIBU
WA SERIKALI, MAHAKAMA NA WADAU
Mhe.
Mgeni rasmi na Wageni Waalikwa, baada
ya kuzungumzia kwa kifupi kuhusu dhana hii ya Fursa ya kupata haki katika mchakato
mzima wa utoaji haki hapa nchini, sasa naomba nizungumzie kipengele cha pili
kama nilivyokwisha dokeza hapo juu. Nini wajibu wa Serikali, Mahakama
na Wadau wa Mahakama kwa ujumla katika mchakato huu wa utoaji haki?.
Mhe.
Mgeni Rasmi na Wageni Waalikwa, hapa nchini fursa ya kupata haki imeendelea kuwa ni ndoto na jambo gumu
kuifikia hususani kwa jamii ambazo ziko pembezoni/jijini na masikini kwa ujumla
katika jamii yetu, japo sasa taratibu imeaanza kuonekana kwa kuwa Serikali na
wadau wake wa maendeleo wameunganisha nguvu zao kwa kuweka mazingira ambayo
yanaruhusu huduma za kisheria kuwafikia wananchi waalioko chini - down to
the grassroots level. Pamoja na juhudi za muda
mrefu za Serikali yetu kuhakikisha kwamba wananchi wanapata fursa ya kupata
haki zinaonekana kuzaa matunda, lakini uhalisia wa mambo ni kwamba fursa hii ya
kupata haki haijazaa matunda kwa namna inayofaa hususani miongoni mwa jamii
inayoishi pembezoni. Mara kadhaa tumesikia habari za kutisha na kusikitisha
zinazoambatana na uvunjaji wa haki za binadamu.
Ili mwananchi apate fursa ya kuufikia
mfumo wa utoaji haki hapa nchini kwa mujibu wa Sheria, Kanuni na Taratibu
tulizonazo, lazima Serikali kwa upande wake, Mahakama na Wadau wenyewe watimize
wajibu wao.
Mhe.
Mgeni Rasmi
naomba nitaje kwa kifupi baadhi ya mambo ambayo ni wajibu wa Serikali, Mahakama
na Wadau.
Ø WAJIBU
WA SERIKALI
(i) Kuhakikisha vyombo vya Serikali
vinashirikiana na kutimiza majukumu yake ipasavyo.
Katika
kuhakikisha fursa ya kupata haki inafikiwa vyombo vya Polisi, Magereza,
Takukuru, Ofisi ya Waendesha mashitaka / Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Ustawi
wa Jamii, Takukuru n.k, vina wajibu mkubwa katika kuhakikisha fursa ya kupata
haki inafikiwa. Kwa mfano ili mshitakiwa
afikishwe Mahakamani ni lazima Polisi
ama Takukuru wakamilishe upelelezi wao kikamilifu na ndipo wanasheria wa
Serikali wanaweza kuendelea na shitaka husika na hatimaye kuipa Mahakama fursa
ya kusikiliza na kutoa uamuzi. Na endapo
chombo kimoja kitashindwa kutekeleza majukumu yake kikamilifu basi fursa ya
kupata haki haiwezi kufikiwa. Serikali
inawajibu wa kuhakikisha vyombo hivi vinatengewa bajeti pamoja na vitendea kazi
vya kutosha ili vitimize majukumu yake kikamilifu.
(ii) Kukuza na kuhamasisha ufahamu wa sheria.
Mhe. Mgeni rasmi na Wageni Waalikwa, ili jamii iweze kuwa na fursa ya kupata
haki inatakiwa kuwa na uelewa wa kutosha juu ya haki na wajibu wao na namna ya
kudai haki hizo. Serikali inawajibu wa
kuhakikisha inawahamasisha na kuwawezesha wananchi kuwa na elimu ya ufahamu juu
ya Sheria za Nchi kupitia vyombo vya habari, vipeperushi, Makongamano, Mikutano
ya hadhara, Kampeni mbalimbali, n.k
(c)
Kujenga na kuboresha miundo mbinu ya Mahakama, Polisi, Magereza na kuajiri
watumishi wa kutosha wanaokidhi vigezo nya utumishi wa umma.
Katika
kuhakikisha wananchi wanapata fursa ya kupata haki, suala la miundo mbinu ya
Mahakama kwa maana ya majengo, Vituo vya Polisi, Magereza pamoja na upanuzi wa
magereza ni jambo la msingi na muhimu.
Suala la kuwa na idadi ya watumishi wanaokidhi vigezo na mahitaji kama
vile Majaji na Mahakimu, watumishi wengine wa Mahakama, Askari polisi, Askari
Magereza, na Wanasheria wa Serikali kwa ujumla ni jambo ambalo Serikali lazima
ilitazame kwa jicho la pekee kwa kuwa ni wajibu wa Serikali kuhakikisha kuwa
inajenga imani kwa jamii tunayoihudumia. Hakika kukosekana kwa huduma za Kimahakama au vituo vya polisi na uhaba wa
watumishi hii inaweza kupelekea wananchi kukosa fursa ya kupata haki au
kusafiri umbali mrefu kuipata. Serikali inawajibu wa kuhakikisha inaboresha
majengo na kuajiri watumishi wa kutosha.
Ø WAJIBU
WA MAHAKAMA
Mhe.
Mgeni na Wageni waalikwa, imani na sifa ya wananchi kwa mahakama
haviwezi kujengwa na kudumishwa kama wananchi hawajui jinsi Mahakama
inavyofanya kazi zake. Wananchi hawana budi kupewa nafasi ya kuelewa vyema
umuhimu wa chombo hiki cha Mahakama katika mchakato mzima wa utoaji haki nchini
na uhuru wake kwa ujumla. Pamoja na mambo mengine, chombo hiki kina wajibu wa:
(i)
Kutenda haki kwa wote na kwa wakati.
Mahakama
kama chombo pekee na kilele cha utoaji haki, ina-wajibu wa kuhakikisha kwamba
wananchi wanakifikia chombo hiki bila kikwazo na inatoa maamuzi kwa wakati na
ufanisi kwa kuzingatia misingi ya haki na usawa. Ibara ya 107A (2) inasema;
“Katika
kutoa uamuzi wa mashauri ya Madai na Jinai kwa kuzingatia Sheria Mahakama
zitafuata Kanuni zifuatazo, yaani;
(a) kutenda
haki kwa wote bila ya kujali hali ya mtu kijamii au kiuchumi,
(b) Kutochelewesha
haki bila sababu ya msingi,
(c) …..
(d) …..
(e) …..
Mhe. Mgeni rasmi, Wananchi hawawezi kukiona chombo hiki cha
Mahakama kama kimbilio la kutatua migogoro yao ikiwa tu maamuzi ya Mahakama
hayatakuwa ya haki na kutolewa kwa wakati. Badala yake wananchi hawa wanaweza
kuwa wanajichukulia sheria mkononi kwa sababu tu yakukosa imani na chombo hiki.
(ii)
Kusimamia maadili ya watumishi wa
Mahakama.
Suala
la kutoa haki linatawaliwa na uaminifu na uadilifu wa hali ya juu kwa Jaji au
Hakimu pamoja na watumishi wa Mahakama. Tunaweza kuwa na Sheria nzuri lakini
kama watendaji hawa na watumishi kwa ujumla watakosa uaminifu na uadilifu,
hakika haki haiwezi kutendeka na wananchi wanaweza kupoteza imani na chombo
hiki na hata kushindwa kwenda Mahakamani kutafuta haki zao kwa hofu ya
kutotendewa haki. Kwa maana hiyo, Mahakama inawajibu mkubwa wa kuhakikisha kuwa
watumishi wote katika ngazi zote wanazingatia maadili ya utumishi wa Umma.
Mhe, Mgeni rasmi na Wageni Waalikwa, kwa kutambua umuhimu wa suala la
maadili, Mahakama ya Tanzania hivi sasa ipo katika mageuzi
mbalimbali ambayo yanalenga katika kuboresha huduma ya utoaji haki nchini.
Mageuzi hayo ni pamoja na Mabadiliko ya Sheria Na. 4 ya Mwaka 2011 ya
Uendeshaji wa Mahakama, lengo kuu likiwa ni kurahisisha huduma ya utoaji
haki ikiwa ni pamoja na kuleta ufanisi katika utekelezaji wa majukumu. Kutokana
na mageuzi haya, hivi sasa kuna Watendaji wa Mahakama katika kila mkoa, ambapo
hatua hii pia imelenga katika kuhakikisha kuwa majukumu ya kiutawala
yanatekelezeka na Watawala na pia yale ya Kimahakama yanatekelezwa na Wasajili
na Mahakimu na hatimaye kurahisisha huduma ya upatikanaji wa haki kwa wakati.
Mhe, Mgeni rasmi na ageni Waalikwa, pamoja na ukweli kwamba hali ya majengo ya Mahakama tunazofanyia kazi mengi ni chakavu na pengine
hayafai kwa ajili ya shughuli za Kimahakama, ni vema sisi watendaji na watumishi kwa ujumla tutambue kwamba Uongozi wa juu wa Mahakama ya Tanzania umejipanga kuboresha majengo yake, ikiwa ni
pamoja na kujenga upya na kukarabati majengo yenye unafuu. Kupitia maadhimisho haya, napenda kutoa rai kwa
watumishi wenzangu katika Mkoa wa Shinyanga na wengine kote Nchini, kufanya kazi kwa bidii ili kujenga imani kwa wananchi
tunaowahudumia. Ninaamini, kama kila mtumishi wa
Mahakama atafanya kazi yake kwa uaminifu na uadilifu itakuwa rahisi kwa
wananchi siyo tu kwenda/kufika
Mahakamani kudai haki zao, lakini pia, Mahakama itakuwa na uwezo wa
kushughulikia kesi husika na kufanya maamuzi ya haki.
Tukumbuke
kwamba kuelimisha jamii juu ya haki na wajibu wao kwa mujibu wa Sheria, Kanuni
na Taratibu tulizonazo inachangia kwa kiasi kikubwa kuleta mwamko kwa jamii kufika
katika vyombo vya kutoa haki kudai haki zao.
Ø WAJIBU
WA WADAU WA MAHAKAMA
Wadau
wa Mahakama ni kundi ambalo linajumuisha wananchi wenye kesi Mahakamani
(wadaawa), Polisi, Magereza, Ofisi ya Waendesha Mashtaka, Mawakili wa
kujitegemea, Taasisi za Serikali na zisizo za Kiserikali, Madalali wa Mahakama,
Takukuru, Ustawi wa Jamii, Mashirika ya Umma, N.G.O’s, Asasi za Kiserikali na Kiraia,
n.k. Kundi hili lina wajibu wa kuelemisha
jamii kujua haki zao na namna ya kuufikia mfumo wa utoaji haki pamoja na kutoa
msaada wa kisheria. Kundi hili linawajibu mkubwa wa kuhakikisha wananchi
wanaelimishwa kiasi cha kutosha juu ya haki zao na sheria za nchi. Pia ni wajibu wa kundi hili kutoa msaada wa
kisheria kwa gharama ya chini ili kuwapa wananchi unafuu wa kupata huduma za
kisheria. Kufanya hivyo, kundi hili lina
nafasi kubwa ya kuisaidia jamii kuwa na uwezo wa kuutumia mfumo wa utoaji haki
kikamilifu. Maeneo ya pembezoni mwa nchi
yetu hasa vijijini watu wamekuwa hawapati fursa ya kupata haki kwa sababu tu
hawana uelewa wa kutosha juu ya haki zao, mbali na kutofahamu sheria, Kanuni na
Taratibu zilizopo. Tatizo la kiuchumi na fedha nalo limechangia kwa kiasi
kikubwa kuwafanya wananchi kukosa haki zao.
Aidha, Asasi za Kiraia zina
wajibu mkubwa wa kutoa elimu ya msaada wa kisheria pamoja na kuwawezesha au
kuwapa uwezo wa Kisheria (Legal empowerment) kwa madhumuni ya
kuwa na ufahamu na kutambua namna ya kutafuta na hatimaye kupata fursa ya
kupata haki zao.
(iv)
HALI HALISI YA FURSA YA KUPATA HAKI KATIKA
MKOA WETU WA SHINYANGA
Mhe. Mgeni na Wageni waalikwa, naomba pia niseme japo kwa ufupi kuhusu
hali halisi ya fursa ya kupata haki katika
Mkoa wetu wa Shinyanga. Katika Mkoa wetu wa Shinyanga fursa ya kupata haki inakabiliwa
na changamoto mbalimbali. Miongoni mwa changamoto hizi ni pamoja na:-
1.
UCHAKAVU WA MIUNDO MBINU YA MAHAKAMA
Kuna uhaba mkubwa wa Majengo ya Mahakama na mazingira yasiyo
rafiki ya kufanyia kazi hususani kwa watumishi wa Mahakama zilizo
pembezoni. Kwa ujumla, suala hili
limekuwa ni kikwazo kwa wananchi kuweza kupata fursa ya kupata haki. Hii
inatokana na ukweli kuwa watumishi wengi wa Mahakama wamekuwa wakiacha kazi au
kufanya kazi katika mazingira magumu.
Matokeo yake Mahakama nyingi zina kosa Mahakimu na kupelekea wananchi
kushindwa kupata fursa ya kupata haki.
2.
RUSHWA
Kama tunavyofahamu, rushwa ni adui wa haki, na rushwa ni
kikwazo cha fursa ya kupata haki katika maeneo yetu ya kazi. Tafiti mbalimbali za hivi karibuni zinautaja
mhimili wa Mahakama kuwa ni wa pili baada ya jeshi la polisi kwa ulaji wa
rushwa. Mtaalam mmoja aitwae Bryan A.
Stevenson ambaye ni Profesa katika Chuo Kikuu Cha New York, Shule ya Sheria
ambae pia ni mwanzilishi na Mkurugenzi wa Taasisi ya Haki sawa huko Marekani,
aliwahi kusema, na nina mnukuu;
“Mfumo wetu utakuhudumia vizuri kama ni tajiri na mwenye hatia, kuliko
ukiwa masikini na usiwe na hatia.” Mwisho
wa Kunukuu.
Na aliyewahi kuwa Rais wa 11 Inchini India (kati ya Mwaka 2002 - 2007) Bw. A.P.J. Abdul Kalam aliwahi kusema maneno haya; na nina-mnukuu;
“Kama
nchi inataka kuondokana / kutokuwa na rushwa na kuwa nchi yenye fikira njema,
kwa dhati ninafikiri kuna watu watatu
katika jamii yetu wanaweza kupelekea kuwa tofuati ambao ni Baba, Mama na
Mwalimu.” Mwisho wa Kunukuu.
Mhe. Mgeni rasmi na wageni waalikwa, wale wanaofanya kazi za kimahakama
watakubaliana na mimi kwamba rushwa
ni kitendo kinachoondoa uhuru wa maamuzi ya kuzingatia misingi ya haki. Rushwa siyo tu imekuwa kikwazo katika
kuhakikisha haki inatendeka, lakini pia, imekuwa ni kikwazo kwa wananchi
kuufikia mfumo wa utoaji haki kwa hofu
kuwa hawataipata au kutendewa haki.
Mbali na watendaji wa Mahakama kwa maana ya Majaji na Mahakimu, kumekuwepo na wimbi kubwa la watumishi
wengine wa mahakama wasio waadilifu na wasio wa watumishi wa Mahakama kudai
kupewa rushwa na wengine kudiriki kutumia majina ya Majaji na Mahakimu kuomba
rushwa. Nichukue fursa hii kuwataka watumishi wote wa Mahakama katika Mkoa
wetu wa Shinyanga na Taifa kwa ujumla
kuzingatia maadili ya utumishi wa Umma na ninaiomba Serikali na Jamii kuwa
mstari wa mbele kukemea rushwa kuanzia ngazi ya familia.
3.
ELIMU JUU YA HAKI, WAJIBU NA SHERIA KWA
WANANCHI
Katika Mkoa wetu wa Shinyanga, sehemu
kubwa ya wananchi waishio vijijini (pembezoni) wamekuwa na uelewa mdogo kuhusu
suala zima la haki zao na wajibu walionao kwa chombo hiki cha Mahakama. Lakini, kwa maeneo ya mijini kwa kiasi kikubwa yameendelea kunufaika na fursa
hii ya kupata habari na kuwa uelewa juu ya haki zao kupitia vyombo vya habari
na Wanahabari wenyewe, Mikutano ya hadhara, Mafunzo maalumu, Vipeperushi, Mbao
za Matangazo, Taasisi za kutoa misaada na ushauri wa kisheria, tofuati na maeneo ya vijijini ambako
fursa hii haipatikani kwa urahisi. Changamoto hii imepelekea wananchi walio
wengi kushindwa kuufikia mfumo wa utoaji haki kwa kwa sababu ya mazingira
waliyonayo.
Napenda kutoa
rai kwako wewe Mhe. Mgeni Rasmi, viongozi wote mliopo hapa, hususani viongozi
wa Halmashauri zetu, Asasi za Kisheria, Wanahabari, viongozi wetu wa vyama vya
siasa, na wote mnaonisikiliza kwa pamoja tushirikiane kutoa elimu na
kuielimisha jamii pamoja na kuiwezesha kuipa elimu ya Kisheria juu ya haki zao
na wajibu wao kwa chombo hiki cha Mahakama kwani kwa namna moja ama nyingine,
hii inaweza kuwa ndiyo tiba na suluhu ya changamoto hii. Baba wa Taifa aliwahi kusema, Inawezekana, Timiza wajibu wako.
MWISHO
Mhe. Mgeni rasmi na Wageni waalikwa, katika kuhitimisha salamu zangu,
napenda kumalizia kwa kusema kwamba ili fursa ya kupata haki iweze kufikiwa, ni
lazima vikwazo kama vikwazo vya kiuchumi, lugha, elimu juu ya haki na Sheria,
n.k. vinaondolewa. Kwa upande wake, Serikali, Mahakama, na Wadau wa Mahakama
wanawajibu mkubwa wa kushirikiana kwa pamoja sambamba na wadau wengine wa
maendeleo katika nyanja ya sheria katika utoaji wa elimu, huduma na misaada ya
kisheria bila malipo kwa jamii ambayo inakipato cha chini kwa maana ya paralegals
and pro bono publico kuhakikisha vikwazo hivyo vinaondolewa na wananchi
wanapata fursa ya kupata haki zao kwa wakati. Lakini pia natoa rai kwa watumishi wenzangu kujipanga vizuri kwa
ajili ya kutekeleza majumu ambayo yako mbele yetu na hasa tukizingatia kwamba
maadhimisho haya yanaashiria mwanzo rasmi wa shughuli za Kimahakama, huku
tukijiandaa kwa ajili ya uzinduzi rasmi wa jengo letu la Mahakama kuu
Shinyanga.
Baada ya
kusema hayo napenda kuwashukuruni nyote kwa usikivu wenu.
Asanteni
Sana na Mungu awabariki.
|