POLISI WAUA MAJAMBAZI WAWILI JIJINI DAR ES SALAAM


Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limefanikiwa kukamata silaha moja aina ya SMG yenye namba BA172288 na risasi 13 wakati wa mapambano makali ya ana kwa ana kati ya majambazi na Jeshi la Polisi.

Taarifa iliyotolewa na jeshi hilo Kanda Maalum ya Dar es salaam, imesema kuwa katika tukio hilo majambazi wawili waliuawa kwa risasi wakati wakijaribu kuwadhuru askari.
 
Tukio hilo lilitokea eneo la Kariakoo mtaa wa Mkunguni na Livingstone saa 3.00hrs usiku  wa jana. Wakati wa tukio hilo umeme ulikuwa hakuna na mlalamikaji alikuwa anatumia taa za kawaida.
 
Mara baada ya kuanza tukio hilo la uporaji wasamaria wema walijulisha Jeshi la Polisi ndipo kikosi maalum cha kupambana na majambazi (ant robbery squared) kilipofika kwa haraka katika eneo la tukio tayari kwa mapambano.
 
Taarifa hiyo inasema kuwa Majambazi hao walistuka na kuanza kuwarushia risasi askari waliokuwa katika gari la Polisi na ndipo sasa kukawa na mapambano ya moja kwa moja kati ya pande hizo mbili kwa kutumia silaha na kurushiana risasi. 

Hatimaye majambazi wawili waliuawa, mmoja anayejulikana kwa jina la ALLAN S/O OCHENG @ ONYANGO, Miaka 24, raia wa Kenya alipatikana na Pass ya kusafiria yenye nambari A1688495 iliyotolewa katika mji wa KISUMU nchini Kenya.
 
Jambazi mwingine aliyeuawa ametambuliwa kwa jina la YUSSUPH S/O HAMIS @ TWALIB, Miaka 46, Mshiraz, Mkazi wa Kariakoo jijini Dar es Salaam.
 
Majambazi wengine waliotoroka baada ya tukio hilo wanaendelea kutafutwa na tunaomba raia wema waendelee kushirikiana na Jeshi la Polisi ili wapatikane.
 
Pamoja na kuuawa kwa majambazi hawa na kukamatwa kwa silaha, pia zimekamatwa pikipiki mbili moja ni SUNLG yenye namba za usajili T249 CMC, rangi nyekundu. Nyingine ni aina ya BOXER yenye namba za usajili MC350 AM rangi nyeusi ambazo zote zilitumiwa na majambazi hao katika tukio.
 
Aidha, Jambazi ALLAN S/O OCHENG @ ONYANGO aliyeuawa amekutwa na simu ya mkononi aina ya TECNO.
 
Majambazi Wengine 9 Sugu Wakamatwa  jijini  Dar
Katika msako mkali unaoendelea jijini Dar es Salaam dhidi ya ujambazi wa kutumia silaha Jeshi la Polisi limekamata majambazi tisa wanaojihusisha na matukio ya uhalifu ya unyang’anyi wa kutumia silaha na makosa ya kuvunja nyumba usiku na kuiba.
 
Oparesheni kali bado inaendelea jijini Dar es Salaam ili kuhakikisha kwamba majambazi wote wanaotumia silaha pamoja na makosa mengine ambayo ni kero katika jamii yanashughulikiwa kikamilifu.
 
Pamoja na mafanikio hayo tunawashukuru raia wema kutokana na juhudi zao za kutoa taarifa mapema zenye kuwa na mafanikio ya kulifanya jiji la Dar es Salaam liendelee kuwashwari.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527