HAYA NDIYO MAGONJWA YANAYOONGOZA KUUA WATU MKOA WA SHINYANGA


Dkt Ntuli Kapologwe


Imeelezwa kuwa magonjwa yanayoongoza kusababisha vifo mkoani Shinyanga ni pamoja na Malaria,Ukimwi,kisukari na shinikizo la damu huku ajali ya pikipiki nazo zikichangia kwa hali nyingine vifo vya watu wengi mkoani Shinyanga.

Hayo yamebainishwa juzi na mganga mkuu wa mkoa wa Shinyanga Dkt Ntuli Kapologwe wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake.

Dkt Kapologwe alisema ugonjwa malaria ni tishio mkoani Shinyanga na ndiyo ugonjwa ambao unaua watu wengi hususani watoto wengi wenye umri chini ya siku 28 na wengine chini ya miaka mitano.

Alisema katika kipindi cha mwezi Januari hadi Desemba watoto 98 wenye umri chini ya siku 28  walipoteza maisha kutokana ugonjwa wa malaria.

Dkt Kapologwe alisema ugonjwa wa UKIMWI pia bado ni tishio mkoani Shinyanga na kwamba watu wengi wakiwemo watoto,vijana na wazee wanaendelea kupoteza maisha kutokana na ugonjwa huo hivyo kuitaka jamii kuepuka mara moja sababu zinachochangia kuambukizwa virusi vya Ukimwi kwa taifa linapoteza nguvu kazi kila kukicha.

Magonjwa mengine yanayosababisha vifo vingi mkoani humo ni ugonjwa wa kisukari na shinikizo la damu,ambapo hivi sasa yanawapata zaidi vijana tofauti na zamani ambapo magonjwa hayo yalikuwa yanadaiwa kuwapata watu wenye umri mkubwa(wazee).

Mganga huyo mkuu wa mkoa wa Shinyanga alisema mbali na magonjwa hayo manne,ajali za barabarani hususani za pikipiki zinachangia kwa kiasi kikubwa vifo vya wananchi wa mkoa huo.

Alisema takwimu zinaonesha kuwa hospitali ya mkoa wa Shinyanga pekee kila siku inapokea mgonjwa mmoja aliyepata ajali ya pikipiki hivyo kuwataka wananchi kuchukua tahadhari wanapoendesha vyombo vya moto barabarani.

Katika hatua nyingine aliwataka wakazi wa Shinyanga kufika katika vituo vya afya,zahanati  na hospitali ili kupata huduma kwani dawa zote muhimu zinapatikana kwa asilimia 98 na watoa huduma wana ujuzi na weledi wa hali juu katika kuhudumia wagonjwa.

“Tumepeleka dawa za kutosha kwenye vituo vyote vya afya,zahanati na hospitali zote,Shinyanga hatuna tatizo la upungufu wa dawa,malalamiko yaliyopo sasa ni wagonjwa kulalamikia baadhi ya wauguzi kuwatolea lugha mbaya”,alieleza Dkt Kapologwe.
Na Kadama Malunde-Shinyanga

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527