VIONGOZI WA CCM WANUSURIKA KUCHOMWA MOTO BAADA YA KUKUTWA WAKIGAWA CHUMVI MTAANI HUKO GEITA

Chumvi iliyozua kizaa zaa huko Geita-Picha na Valence Robert-Malunde1 blog Geita

Baadhi ya mapakiti ya chumvi yalikuwa yanagawiwa kwa wananchi-Picha na Valence Robert-Malunde1 blog Geita

Wananchi wakiwa nje ya nyumba waliwafungia wafuasi wa CCM -Picha na Valence Robert-Malunde1 blog Geita

Wananchi wakiwa eneo la tukio-Picha na Valence Robert-Malunde1 blog Geita

Wananchi wakiwa eneo la tukio-Picha na Valence Robert-Malunde1 blog Geita

Watu 10 wanaodaiwa kuwa ni wafuasi wa Chama Cha Mapinduzi(CCM),wakiwemo mabalozi wa nyumba kumi wakazi wa mtaa wa Mkoani kata ya Kalangalala Wilayani Geita Mkoa wa Geita wamenusurika kuuawa kwa kuchomwa moto na wananchi wenye hasira kali baada ya kuwakuta wakigawa chumvi kwa wananchi kama njia ya kuwashawishi kuchagua viongozi wa chama chao katika uchaguzi wa serikali za mitaa utakaofanyika Desemba 14 mwaka huu.

Katika tukio hilo,vigogo wa CCM mkoa wa Geita akiwemo mbunge wa viti maalumu Vicky Kamata walichafua hali ya hewa baada ya kufika eneo hilo la tukio kwa lengo la kuwakingia kifua watuhumiwa na kusababisha upepo kuchafuka zaidi hali iliyopelekea polisi kutishia kuondoka eneo hilo ili wananchi wajitawale.

Tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia Desemba 10 mwaka huu majira ya saa 3:30 usiku ambapo jeshi la polisi lilifika eneo hilo na kutumia nguvu ya ziada kuwashawishi wananchi wasijichukulie sheria mkononi kwa kuwapiga na kuwachoma watu hao mbele ya vyombo vya dola.

Mwandishi wa malunde1 blog mkoani Geita Valence Robert alipigiwa simu majira ya saa 2:30 usiku na  baadhi ya wananchi mwandishi wa wakimtaka afike eneo la tukio kushuhudia tukio hilo na bila kuchelewa mwandishi wetu alifika eneo hilo na kukuta wananchi hao wakiwa wamefura hasira.

Mwandishi wetu alishuhudia  wananchi wakiwa wamewafungia kwa nje watuhumiwa hao waliokuwa ndani ya nyumba ya balozi wa chama hicho tawala.
‘’Bora mwandishi umekuja hii ni nyumba ya balozi wa CCM na ndani ya nyumba hii tumewafungia mabalozi wake na wananchi mbalimbali ambao tumewakuta wakigawa chumvi kwa wananchi",walieleza.

 "Na hapa unapotuona tumekupigia simu uje uchukue picha ya majivu ya hawa watu maana tunataka kuiteketeza kwa moto nyumba hii tumechoka na hawa watu kutugeuza kuku wa kienyeji’’alisikika mkazi mmoja wa eneo hilo akizungumza kwa jazba na mkononi akiwa na kidumu cha mafuta ya petrol.

Kufuatia hali hiyo,mwandishi wa habari hizi aliwasihi wananchi hao kuacha kuchukua hatua hiyo ya kinyama na badala yake aliwataka waite polisi iwachukue na kuwafikisha kwenye vyombo vya dola ambapo walikubali na kuamua kuita polisi waliofika bila kuchelewa.

Hata hivyo muda mfupi baada ya polisi kuwasili eneo hilo,baadhi ya vigogo wa chama hicho mkoa wa Geita akiwemo mbunge wa viti maalumu mkoa wa Geita Vicky Kamata,mjumbe wa halmashauri kuu ya CCM Taifa Leonald Bugomola,Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Geita Muhoja Mapande, Katibu mwenezi wa CCM Wilaya ya Geita aliyejulikana kwa jina moja la Masele waliwasili eneo hilo.

Viongozi hao walianza  kuwakingia kifua watuhumiwa hao wasipelekwe polisi hali iliyosababisha upepo uliokuwa umetulia eneo hilo kuvuma tena na wananchi kutishia kupiga yowe ili wananchi wakusanyike na kuwachoma moto watu hao.

Aidha polisi waliamua kutumia lugha za ukali wakiwataka vigogo hao wa CCM kuwa wapole huku wakitishia kuondoka eneo hilo ili wananchi wafanye watakavyo kutokana na vigogo hao kutaka kutumia vyeo vyao na jina la chama tawala kuwafundisha kazi polisi.

‘’Mmekuja hapa mmekuta wananchi wametulia lakini nyinyi mnataka kuleta fujo na kutuona sisi hatufai,sasa kama ni hivyo tutaondoka hapa tuwaache wananchi watimize adhima yao na tuone kama mtaweza kukabiliana na nguvu ya umma".

"Hebu kuweni wasitaarabu tuwachukue hawa watu kwa amani tuwapeleke kituoni na kama kuna mtu anashida na hawa watuhumiwa aje kituoni’’,alisikika askari mmoja aliyefahamika kwa jina la Dani akipiga mkwara vigogo hao ambao waliamua kuwa wapole.

Baadaye wanachama hao walifikishwa kituo cha polisi Wilaya ya Geita wakiwa na pakiti zao za chumvi kama kidhibiti.

Kwa mjibu wa mkuu wa upelelezi wa makosa ya jinai wilaya ya Geita John Maro aliyekuwa eneo la tukio hilo alisema watuhumiwa wanashikiliwa na jeshi hilo kwa mahojiano zaidi na upelelezi ukikamilika watafikishwa mbele ya sheria kujibu tuhuma zinazowakabili. 

Na Valence Robert-Malunde1 blog Geita 

Mtandao Huu Unakujali,Ni Wako!! Tunataka Tukutumie Habari zetu Zote Mara Tu Tunapozipandisha Mtandaoni.Kujiunga nasi Bonyeza Hapa Sasa Hivi ><<VITUKO>>,"MAPENZI",<<HABARI MSETO>>  Pia waweza kuwasiliana na Malunde kwa simu/Whatsapp +255 688 405 951 Kama una habari ,picha au Tangazo

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527