JWTZ>>"MSANII DIAMOND HAKUWA NA RUHUSA YA KUVAA SARE ZETU"

 jwtz
JESHI la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), limesema kuwa mwanamuziki wa kizazi kipya, Nassib Abdul maarufu ‘Diamond Platinumz’, aliyetinga na sare za jeshi jukwaani kwenye tamasha la Fiesta, hakuwa na kibali cha kuvaa nguo hizo.

Jeshi hilo ambalo bado linaendelea na uchunguzi, limesema kwa kawaida JWTZ haiwezi kutoa nguo au vifaa vyake kwa ajili ya maonesho ya wanamuziki au shughuli nyingine yoyote zaidi ya matumizi ya jeshi.

Kauli hiyo ilitolewa jana na Ofisa Mnadhimu wa Mkoa wa Polisi Kinondoni, Mrakibu Mwandamizi (SSP), Boniventure Mushongi.

Alisema hakuna kibali kinachotolewa na jeshi lolote kwa nguo au vifaa vyake kutumika na watu wasio wanajeshi.

“Jeshi haliwezi kutoa kibali cha nguo zake kutumika jukwaani, hata hao wasanii wanaoonekana kuvaa nguo za jeshi majukwaani wanakiuka sheria,” alisema SSP Mushongi.

Hata hivyo, alipoulizwa kwa nini jeshi la Polisi lilishindwa kuchukua hatua siku ya tukio, SSP Mushongi alisema kwa hali ilivyokuwa, isingekuwa rahisi kufanya hivyo na huenda zingetokea fujo.
“Jeshi la Polisi linafanya kazi kwa weledi. Lingeweza kumchukulia hatua siku ile ile aliyopanda jukwaani na mavazi yale, ila haikuona madhara kwa wakati huo shughuli zinaendelea.. endapo hali ile ingetokea mikoani huko, msanii huyo angechukuliwa hatua hapo hapo,” alisema.
SSP Mushongi, aliongeza kuwa hatua ya wasanii nchini kupenda kuvaa mavazi ya majeshi ni ukiukwaji wa sheria na elimu zaidi inahitajika.

Hata hivyo, habari zaidi zinasema wanenguaji wa mwanamuziki huyo, wamekamatwa na kuhojiwa na Polisi wa kituo hicho cha Oysterbay, kwa tuhuma za kuvaa sare za JWTZ.

Wengine walioshikiliwa ni pamoja na meneja wake Hamis Taletale ‘Babu Tale’ ambaye ameshaachiwa baada ya kuhojiwa.

Hata hivyo, awali vyanzo mbalimbali vya habari vilivyoifikia Tanzania Daima, vilieleza kuwa, Babu Tale alijisalimisha Polisi Oysterbay juzi majira ya jioni na baada ya kuhojiwa, aliswekwa mahabusu. Babu Tale alipoulizwa alipo Diamond, alisema amesafiri nje ya nchi mara baada ya onyesho la Fiesta.

Hata hivyo, Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kinondoni, Kamishna Msaidizi (ACP), Camillus Wambura, alisema bado hajapata taarifa ya kukamatwa kwa meneja huyo pamoja na wanenguaji hao, kwani shauri hilo l ipo kwenye uchunguzi chini ya Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa.

via>>Tanzania Daima

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527