Haya Sasa!! KUTANA NA VYAKULA VINAVYOWEZA KUKULETEA UGONJWA WA SARATANI


UTAFITI mbalimbali uliokwishafanywa unaonyesha kuwa magonjwa mengi ya saratani (cancer) yanatokana na vyakula tunavyokula kila siku katika maisha yetu. Katika siku za hivi karibuni, ongezeko la magonjwa haya limekuwa kubwa kwa sababau vyakula vinavyosababisha magonjwa hayo, ndivyo vinavyoliwa sana kuliko vile vinavyozuia.
 Wiki iliyopita tuliwaorodheshea baadhi ya vyakula vinavyoaminika kusaidia kuzuia magonjwa ya kansa ambapo wiki hii tunawaletea orodha ya vyakula vinavyoaminika kuongoza kwa kuwa chanzo cha magonjwa hayo hatari:
VYAKULA VYA KUKAANGA
 Vyakula vingi vinavyotayarishwa kwa kukaangwa kwenye mafuta yenye moto mkali huwa na madhara kiafya na miongoni ma madhara hayo ni pamoja na kusababisha kansa ya kwenye mfuko wa uzazi. Vyakula hivyo ni pamoja na chips na vyakula vingine vinavyopikwa kwa kukaangwa kwenye mafuta.
VYAKULA VYENYE CHUMVI NYINGI
 Vyakula vyenye chumvi nyingi vimebainika navyo kusababisha kansa. Vile vile inaelezwa kuwa chumvi huwa kama chakula kwa bakteria wa kansa tumboni. Kansa ya tumbo inadaiwa kuua watu wengi nchini Japan kutokana na jamii hiyo kupenda sana vyakula vyenye chumvi nyingi. Miongoni mwa vyakula vyenye chumvi nyingi ni vile vya kusindika, kama vile nyama za makopo, maharage, n.k
SUKARI
 Matumizi mabaya ya sukari yanaelezwa kusababisha kansa. Kama tujuavyo, kuna aina mbalimbali za sukari lakini sukari hatari zaidi ni zile zinazowekwa kwenye vinywaji mbalimbali, zikiwemo soda, juisi za ladha ya matunda ambazo huwa na kiwango kingi cha ‘fructose’ ambayo inaelezwa kusababisha saratani ya kongosho.
 Vile vile sukari kwa ujumla wake hairuhusiwi kutumiwa na mtu ambaye tayari amegundulika kuwa na kansa kwa sababu chakula cha chembechembe za saratani mara nyingi huwa ni sukari. Kwa matumizi mengine ya kawaida, sukari inatakiwa kutumiwa kwa kiwango kidogo sana katika vinywaji au vyakula tunavyotumia, tofauti na baadhai ya watu wanavyoweka sukari nyingi ili kupata utamu zaidi.
NYAMA ILIYOIVA SANA
 Upikaji wa nyama kwa muda mrefu na kwenye moto mkali (high temperatures) husababisha aina fulani ya kemikali inayojulikana kitaalamu kama ‘heterocyclic aromatic amines’. Utafiti wa hivi karibuni uliofanywa na Chuo Kikuu cha Utah (University of Utah), umeonesha kwamba watu wanaopenda kula nyama zilizoiva sana, wako hatarini zaidi kupatwa na saratani ya njia ya haja kubwa (Rectal Cancer). Hivyo inashauriwa unapopika nyama, usipike kwenye moto mkali na kuiva kupita kiasi.
POMBE
 Unywaji wa pombe kupita kiasi nao unaelezwa kusababisha aina nyingi ya saratani, kwa wake kwa waume. Aina ya saratani zinazodaiwa kusababishwa na pombe ni pamoja na satarani ya mdomo, ini, utumbo na koromeo, ambazo ndizo zinazoua watu wengi hivi sasa nchini Marekani.
NYAMA NA MAFUTA
 Utafiti uliofanywa na Chuo Kikuu cha Havard nchini Marekani, umegundua kwamba watu wanaopenda kula nyama kila siku wako hatarini kupatwa na saratani ya utumbo kuliko wale wanaokula mara moja moja. Pia baadhi ya mafuta ya wanyama na yale yanayowekwa kwenye ‘baga’ au ‘cheese’ huweza kusababisha kansa.
 Vile vile ulaji wa vyakula vilivyotengenezwa kwa kuchanganya na nyama zilizosindikwa au kuhifadhiwa kwa matumizi ya muda mrefu husababisha saratani pia. Vyakula hivyo ni pamoja na ‘soseji’ ambazo hupendwa na watu wengi. Pia mikate ya nyama ‘hot dogs’ nayo ni chanzo cha magonjwa ya saratani.
VYAKULA VYA UNGA MWEUPE
Vyakula vyote vinavyopikwa kutokana na unga uliokobolewa na kuondolewa virutubisho vyake vyote na kuwa mweupe, vinaelezwa kuchangia magonjwa ya saratani kwa kiasi kikubwa. Vyakula hivyo ni pamoja na ‘donati’ (doughnuts), maandazi, mkate mweupe, n.k

 Mwisho, licha ya kuepuka ulaji wa vyakula vilivyotajwa hapo juu, unatakiwa kuzingatia ulaji wa vyakula asilia vitokanavyo na mimea, mboga za majani na matunda kwa wingi kila siku. Utaona kwamba adui mkubwa wa afya zetu ni vyakula vyote vya kusindika na vile vya kutengenezwa viwandani au vile ambavyo wakati wa utayarisjaji wake huondolewa virutubisho vyake vya asili.
SASA USISUMBUKE TENA KUPATA HABARI ZETU,BONYEZA TU HAYA MANENO TUKUTUMIE HABARI ZETU ZOTE

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527